NA ISSA BIN MARIAM
nilizaliwa sitini na saba
nimefikisha hamsini na saba
nilizaliwa Arusha
jiji kasoro bahari
nikazikwa Zanzibar
kisiwa kinachoelea baharini
naitwa majina mengi
natambulika kwa sifa moja
waasisi huniita Azimio la Arusha
makada Azimio la TANU
wajipendekezao hunipamba Azimio la Nyerere
wajinga hunikejeli Azimio la Mussa
naitwa majina mengi
natambulika kwa sifa moja
mwiba kwa wanyonyaji
maua kwa wanyonge
kero kwa fanyiwakazi
matumaini kwa wafanyakazi
nilizaliwa hospitali ya Mapambano
nikakulia kiwandani MountCaramel
mjukuu wa MamaNtilie
mpendwa wa hohehahe
uhai wangu uliwasumbua
ukuaji wangu uliwatesa
siku na mchana
bila mapumziko, bila raha
gizani na vichakani
wakapanga wakapangua
mipango yao michafu ya kuniua
hatimaye wakanizamisha baharini Hindi
endeleeni kuipa barabara zenu
5-star zenu, viwanda vyenu, miradi yenu
jina la mhenga wangu
eti mnamuenzi kwa kumjengea sanamu
wakati mnamdhalilisha kwa kubomoa usanifu
wa Taifa lililojengwa kwa jasho na damu.
mzimu wangu utaendelea kuwatesa
fikra zangu zitaendelea kuwasumbua
nitafufuka kwa majina ya kidigitali
nitawafuata hekulini
nitahamahama mitandaoni
nitaimba hotelini
05/02/2024
Swadakta
Asante Profesa Issa bin Mariam
LikeLike